HABARI KATIKA PICHA
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony Mtaka (kushoto) na Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Fatuma Mganga (kulia) wakimkabidhi Balozi wa Namibia nchini Tanzania ,Mhe. Lebius Tobius Kitabu cha Muongozo wa Uwekezaji kwenye Mkoa wa Dodoma
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony Mtaka (kushoto) na Balozi wa Namibia nchini Tanzania ,Mhe. Lebius Tobius wakiteta jambo wakati balozi huyo alipomtembelea Mhe. Mtaka ofisini kwake
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony Mtaka (kulia) na Balozi wa Namibia nchini Tanzania ,Mhe. Lebius Tobius (kushoto) wakiwa kwenye mazungumzo, katikati ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Fatuma Mganga
Picha ya pamoja kutoka kushoto: Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony Mtaka, Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Fatuma Mganga na Balozi wa Namibia nchini Tanzania ,Mhe. Lebius Tobius
Picha ya pamoja kati ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony Mtaka, Balozi wa Namibia nchini Tanzania ,Mhe. Lebius Tobius, Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Fatuma Mganga na Maafisa wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
.......................................................................................................................
RC MTAKA AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA BALOZI WA NAMIBIA NCHINI TANZANIA MHE. LEBIUS TANGENI TOBIUS
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Anthony Mtaka, katikati ya Wiki amekutana na kufanya Mazungumzo na Balozi wa Namibia hapa nchini Mhe. Lebius Tangeni Tobius ambapo wamekubaliana kushirikiana kwenye maeneo ya Sekta ya Mifugo, Elimu na Sekta Binafsi za Tanzania na Namibia ili kukuza masuala ya uwekezaji na biashara.
Mazungumzo hayo yamefanyika ofisini kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma ambapo Viongozi hao wawili wamekubaliana kushirikiana kwenye eneo la mifugo hususani uongezaji tija ya uzalishaji mifugo (ng’ombe) na uongezaji thamani wa mazao ya mifugo ikiwemo nyama, maziwa na ngozi kwa kuzingatia uzoefu walionao Namibia katika sekta ya mifugo na fursa kubwa iliyopo Mkoani Dodoma kwa kuwa na idadi kubwa ya mifugo.
Viongozi hao wawili pia wamekubaliana kukuza ushirikiano katika sekta ya Elimu ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Mtaka amemueleza Balozi Tobius kuwa uboreshaji wa hali ya Elimu ni kipaumbele chake namba moja Mkoani Dodoma na kwamba Dodoma ina fursa kubwa kwa kuwa na Chuo Kikuu cha Dodoma ambacho ni kikubwa Afrika Mashariki hivyo kwa kushirikiana na Vyuo Vikuu vya Namibia wataanzisha program za kubadilishana wanafunzi na wataalamu mbalimbali wa vyuo ili kubadilishana uzoefu na utaalamu.
Katika kukuza uwekezaji na biashara, Mhe. Mtaka na Balozi Tobius wamekubaliana kuimarisha mahusiano na mashirikiano kati ya Sekta binafsi ya Namibia na Tanzania hususani katika Mkoa wa Dodoma, ambapo wamekubaliana kuandaa Kongamano litakalofanyika Mkoani Dodoma likihusisha sekta binafsi za pande hizo mbili na maonesho ya bidhaa zinazozalishwa na pande hizo mbili ili kuona maeneo wanayoweza kushirikiana kwa pamoja.
Mhe. Mtaka alitumia fursa hiyo ya mazungumzo na Balozi Tobius kumualika kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo nchini Tanzania vyenye sifa za kipekee Duniani kama vile Mlima Kilimanjaro, Hifadhi za Taifa za Serengeti na Ruaha ili kupitia yeye awaalike Watalii kutoka Namibia kuja Tanzania,
Katika hatua nyingine viongozi hao wawili wamekubaliana kuanzisha mahusiano ya kindugu ya mikoa miwili ya Omusati nchini Namibia na Dodoma nchini Tanzania kwa kutambua kuwa Mkoa wa Omusati una sifa na historia ya kipekee kwa kuwa ndio Mkoa ambao chama cha ukombozi wa Namibia cha SWAPO kilizaliwa huku Dodoma ikiwa ni Makao Maku ya Tanzania, Chama Tawala cha CCM na Serikali imehamishia shughuli zake hapa Dodoma.
Kwa mijubu wa Viongozi hao wawili, Mahusiano kati ya Mkoa wa Omusati Namibia na Dodoma Tanzania yanaendeleza ushirikiano na undugu wa kihistoria uliokuwepo baina ya Tanzania na Namibia tangu enzi za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Bara la Afrika ambapo Tanzania ilichangia kwa kiasi kikubwa katika harakati hizo za ukombozi na kuwa viongozi wengi wa harakati za ukombozi wa nchi za Kusini mwa Afrika waliishi na kupata mafuzo hapa nchini Tanzania.
Jengo la Mkapa (Mkapa House) Barabara ya Hospitali ya Mkoa
Anuani ya Posta: 914 DODOMA
Simu: +255 26 232 4343/232
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@dodoma.go.tz
Hakimiliki©2016 GWF . Haki zote zimehifadhiwa.